HomeResourcesSabbath School quarterly

Nafasi ya Biblia

18/04/2026

Somo la Juma Hili

Omb. 3:22, 23; 2 Tim. 3:15-17; Yohana 17:17; Efe. 1:13; Zab. 119:11; 1 Kor. 2:14.

Fungu la Kukariri

“Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo” (#Ebr. 4:12#).

Biblia. Sina shaka unayo nakala lau moja au pengine nakala nyingi.

Katika historia yote, kitabu hiki chenye thamani kimenakiliwa kwa siri, kimesafirishwa kisiri, na kupigwa marufuku. Ni kitabu kilichochapishwa kwa wingi zaidi ulimwenguni katika lugha yoyote, na pia moja ya vitabu vikongwe zaidi. Baadhi ya watu wamekufa ili kuilinda Biblia.

Biblia iko wapi maishani mwako? Je, unaisoma au huwa inakaa tu kando ya kitanda chako kwenye kasha la vitabu ikikusanya vumbi? Je, maisha yako yana shughuli nyingi sana kiasi cha kutokukupatia muda wa kujifunza Neno la Mungu au unajisikia kuchoka sana kiasi cha kutoweza kufungua kurasa zake?

Neno la Mungu li hai nalo lina nguyu, na Mungu anakuita ili uiruhusu inene moyoni mwako, kukutia moyo, kukupatia changamoto na kukubadilisha, na kukupatia mwongozo na matumaini.

Biblia si tu kitabu cha kitaaluma au mkusanyiko wa visa vya kale. Badala yake, ni taarifa nzuri, ya kina kabisa ya jinsi Muumba wa ulimwengu anavyojitahidi kutuvuta karibu na Yeye. Ikiwa unatamani kukua katika uhusiano wako na Mungu, jambo lililo bora kabisa uwezalo kufanya ni kujisalimisha katika kutumia muda ulio bora pamoja Naye kila siku katika maombi, kusoma Neno Lake lililovuviwa, na kusalimisha nia yako kwa kile Neno linachofundisha.

Jifunze somo la juma hili kwa maandalizi ya Sabato ya Aprili 25.