HomeResourcesSabbath School quarterly
Hali ya Moyo
23/04/2026
Uwezo wetu wa kupokea maelekezo ya Neno la Mungu (Ayubu 22:22) unategemea kwa kiasi kikubwa namna hali ya moyo wetu ilivyo tunapoijia Biblia. 1 Wakorintho 2:14 inalielezeaje hili?
Kuwa na utambuzi wa kiroho kunamaanisha kuwa na ufahamu wa kiroho na uelewa. Hivyo basi inaleta maana kwamba mtu aliye na nia ya kiroho iliyofunguka ataelewa mambo kwa namna tofauti sana asomapo Biblia kuliko mtu ambaye nia yake imefungika. Mtu anayefikiri kwamba Biblia ni upumbavu hatatafuta ukweli katika kurasa zake.
Neno la Mungu linatenda kazi ndani yetu tunapoamini. Unapoifungua biblia yako na kuamini kwamba Mungu analo jambo la kukuambia kupitia katika maneno ya kurasa zake, hakika atanena nawe na kutenda maishani mwako. Lakini kwa kiasi kikubwa hivyo, hilo linategemea imani yako na matarajio yako. Habari njema ni kwamba ikiwa imani yako ni ndogo, Mungu anaweza kusaidia katika kuikuza (Marko 9:24), hata ikiwa ni ndogo kama punje ya haradali (Luka 17:6).
Moja ya makusudi makuu ya Biblia ni kunena ukweli maishani mwetu kuhusu hali ya uhusiano wetu na Mungu na jinsi ya kuuimarisha. Kama moyo wako uko wazi kwa Roho Mtakatifu, unapolikabili Neno kwa unyenyekevu, daima utatoka ukiwa umebadilishwa, ingawa mtu anaweza asitambue hili siku kwa siku, kwani badiliko la namna hii na ukuaji mara kwa mara huwa kwa namna ya kuongezeka. Lakini ikiwa tutang’ang’ania hali yetu ya kutojali na dhambi na hatuko radhi kubadilika, usomaji wa Biblia hautatupatia manufaa sana. Roho Mtakatifu anatusukuma tusogee karibu zaidi na Yesu Kristo. Je, tunataka kusogea karibu zaidi: Ikiwa ndivyo, tunakuwa “tumehikimishwa hata upate wokovu” (2 Tim. 3:15), nasi tutaona mambo ambayo kamwe hatukuwahi kuyawaza.