HomeResourcesSabbath School quarterly
Jifunze zaidi
24/04/2026
Kama ukitafakari maneno ambayo umeyasema kwa saa 24 zilizopita, ungeyatathminije? Je, yalikuwa ya upendo, mema, ya furaha, yanayoinua, yaliyoonesha kuvunjika moyo, kuchoka, kufadhaika, hasira, usengenyaji, au yenye kijicho na nia mbaya? Biblia inasema, “Kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake” (Mt. 12:34). Tukiwa na takataka mioyoni mwetu, huwa ndizo zitokazo katika maneno yetu.
Sote tumepitia hisia za kufadhaika, uchovu, au msongo, na hali hiyo ya akili hubadilisha kile kinachotoka midomoni mwetu (mara nyingi maneno ambayo tunayajutia baadaye). Kinyume chake, wakati mioyo yetu inapojaa upendo kwa ajili ya mtu fulani, huo hutiririka kupitia katika maneno yetu.
Kwa namna hiyo hiyo, Neno la Mungu linanena juu ya moyo Wake na makusudi Yake kwa ajili yetu. Inashangaza kufikiria kwamba maneno haya haya, yanayotoka moja kwa moja kwenye moyo wa Mungu, tunayo viganjani mwetu kwenye Biblia. Ni jambo la kushangaza kweli kuona nguvu ya maneno ya Mungu ilivyo tawala kwenye historia yote.
“Ni jambo moja kuichukua Biblia kama kitabu chenye mafundisho ya maadili mema, kukisikiliza pale tu linapoendana na wakati na hali yetu duniani; na ni jambo lingine kutambua neno hilo kama hakika neno la Mungu aliye hai, neno ambalo ni uhai wetu, neno lipasalo kutawala matendo yetu, maneno yetu na mawazo yetu. Kulichukulia neno la Mungu kama chochote kilicho tafouti au pungufu ya hivyo ni kulikataa. Na kulikataa huko kwa watu wanaodai kuliamini, ndicho chanzo kikuu cha kutokuamini na kukosa maadili kwa vijana.” — Ellen G. White, Elimu ya Kweli, uk. 211, 212.
Masawali ya Kujadili
Muhtasari: Biblia ni hai na ina nguvu, na kuisoma ni msingi wa kukuza uhusiano wetu na Mungu. Si tu kwamba inatufundisha kuhusu tabia ya ajabu ya Mungu na mwingiliano Wake na wanadamu katika historia yote ya dunia—pia inazungumza na kila mmoja wetu leo tunapoifikia kwa unyenyekevu.